Wednesday, April 29, 2020

WAKILI MUSSA KWIKIMA (1939 –  2020)
KATIBU TUME YA WAISLAM YA MGOGORO WA EAMWS, 1968
Unaanzaje kuandika historia ya mtu kama Mussa Kwikima katika Mgogoro wa EAMWS?

Unaanzaje?

Historia ya Mussa Kwikima ni historia ya Waislam baada ya uhuru mwaka wa 1961 walipokuwa wakipambana na changamoto mpya baada ya ile ya changamoto ya ukoloni wa Waingereza. Changamoto ya ukoloni wa Muingereza Waislam waliikabili vizuri wao wakiwa mstari wa mbele wakipanga mikakati ya kila aina kuhakikisha kuwa ukoloni unatokomezwa na kwa hakika ulitokomezwa. Nusu karne imepita hakuna anaejua historia ya wazalendo hawa. Wenye madaraka na elimu ya kuitafiti historia hii wanaiogopa.

Unaanzaje kuandika taazia ya mtu kama Mussa Kwikima na historia yake kama mwanasheria kijana, Jaji ya Mahakama Kuu na mmoja katika wazalendo waliopigana kutetea haki za Waislam baada ya uhuru?

Wakati wa Mussa Kwikima ulikuwa wakati wa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Ulikuwa pia ni wakati wa Mufti Sheikh Hassan bin Ameir mufti wa Tanganyika kiongozi wa juu wa Waislam aliyempokea Nyerere na waongoza Waislam katika umoja wa wananchi kupigania uhuru wa Tanganyika.

Wakati wa Mussa Kwikima ulikuwa wakati wa Abeid Amani Karume Rais wa Zanzibar na Makamu wa Rais wa Kwanza wa Tanzania.

Wakati wa Mussa Kwikima ulikuwa wakati wa Said Ali Mswanya, Waziri wa Mambo ya Ndani, wakati wake ulikuwa wakati wa Hamza Aziz, Inspector General of Police (IGP).

Wakati wa Mussa Kwikima ulikuwa wakati wa Sheikh Abdallah Chaurembo na Sheikh Kassim Juma wote wanazuoni wanafunzi wakipiga goti katika darsa za Sheikh Hassan bin Ameir.

Wakati wa Mussa Kwikima ulikuwa wakati wa Tewa Said Tewa na Bi. Titi Mohamed tayari wameshapoteza nafasi zao za uongozi katika serikali na TANU, Tewa akabakia kuwa Rais wa EAMWS upande wa Tanzania Makamu Mwenyekiti wake akiwa Bi. Titi Mohamed.

Pamoja na viongozi hawa walikuwapo pia Suleiman Kitundu na Rajab Diwani wajumbe wa Kamati Kuu ya TANU waliokuwa sikio analosikizia Mwalimu Nyerere.

Hawa wote niliowataja wanahusika kwa namna moja au nyingine na historia ya Mussa Kwikima. Historia ya Mussa Kwikika haikamiliki bila ya kuwataja watu hawa.

Lakini ukipenda unaweza ukawaongeza watu hawa wengine – Bilal Rehani Waikela muasisi wa TANU Tabora na Katibu wa EAMWS, Rashid Kayugwa na Geofrey Sawayya.

Hawa wawili wa mwisho walikuwa watumishi katika vyombo vya Usalama vile vya siri na vya dhahir.

Unaweza pia ukawaongeza Benjamin Mkapa Mhariri wa gazeti la TANU The Nationalist na Martin Kiama Mkurugenzi wa Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD).

Kati ya mwaka wa 1963 hadi kufikia mgogoro wa EAMWS mwaka wa 1968 yalitokea mengi.

Mwaka wa 1963 Baraza la Wazee wa TANU chini ya Mzee Iddi Tulio lilivunjwa kwa tuhuma za ‘’kuchanganya dini na siasa,’’ tuhuma iliyopekea Mweyekiti wa  kwanza wa Baraza la Wazee afukuzwe TANU mwaka wa 1958.

Mwaka wa 1964 masheikh wengi waliwekwa kizuizini kufuatia maasi ya wanajeshi.

Mwaka wa 1965 katika Uchaguzi Mkuu, Tewa Said Tewa na Titi Mohamed walishindwa katika kura za Ubunge, Tewa Kisarawe na Bi. Titi Rufiji.

Yote haya yalimpita kijana Mussa Kwikima kama mambo ya kawaida. Hakujua kuwa zote zile zilikuwa ishara ya jambo kubwa na zito litakalomalizikia kwa kuvunjika EAMWS na kusimamisha si ujenzi wa EAMWS peke yake bali na mipango yote iliyokuwa ikiendelea ya kujenga shule athari ambayo hadi leo inaonekana.

Kijana mdogo Mussa Kwikima alyaona yale tu yaliyokuwa hadhir mbele ya macho yake.

Mussa Kwikikima wala katika fikra zake haikumpitikia kuwa haya yaliyokuwa yakitokea yeye hayajui, yote yalikuwa yanatengeneza jukwaa kubwa ambalo yeye atakujakuwa mmoja wa waigizaji wa mchezo uliokuwa unatayarishwa baina ya wanasiasa ndani ya TANU na serikali na viongozi wa EAMWS ikiongozwa na Sheikh Hassan bin Ameir na Tewa Said Tewa na Waislam kwa ujumla wao wakiwa watazamaji.

Waislam kwa hakika walikuwa kama watazamaji kwani mchezo ulipokuwa unachezwa kwenye jukwaa hawakushangilia wala hawakuonyesha kuwa mchezo ule haukuwa na mvuto wowote.

Ilikuwa kama vile hawajui nini kinatendeka, nini wanatakiwa kufanya na nini hatima ya mchezo ule.

Mgogoro wa EAMWS ulianza mara tu baada ya Mwalimu Nyerere kuweka jiwe la msingi tayari kwa ujenzi wa Chuo Kikuu Cha Waislam kilichokuwa kinajengwa na EAMWS.

Hii ilikuwa miezi migumu sana kwa Mussa Kwikima na kwa Waislam.

Asubuhi akiamka Mussa Kwikima atasikiliza tarifa ya habari ya RTD na baada ya hapo atasoma The Nationalist habari kuu katika vyombo vyote hivyo ikiwa ni Mgogoro wa EAMWS. Wakati wa mgogoro huu Mussa Kwikima alikuwa bado kijana mdogo wa miaka 29 ndiyo kwanza kamaliza Chuo Kikuu kama Mwanasheria.

Mgogoro huu ulimkuta Mussa Kwikima katika ndoto za ujana na matumaini makubwa katika maisha yake ya kulitumikia taifa lake changa la Tanzania kama mwanasheria. Mussa Kwikima alikuwa mmoja wa wanafunzi wasiozidi 10 waliohitimu katika kundi la kwanza katika Idara ya Sheria Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam Mtaa wa Lumumba.

Tatizo la EAMWS lilianza mara tu baada ya uhuru ndani ya Halmashauri Kuu ya TANU mwaka wa 1963 Nyerere alipopambana na Bi. Titi katika mjadala ulioletwa na Selemani Kitundu na Rajab Diwani kuhusu nafasi ya Aga Khan Tanganyika kama Patron wa EAMWS.

Baadae mwaka huo 1963 katika mkutano wa EAMWS uliofanyika Dar es Salaam lilijitokeza kundi dogo ndani ya EAMWS kikidai Tanganyika ijitoe katika umoja ule ili iundwe jumuia mpya.

Mzee Waikela anasema fikra hizi hazikuwa fikra za Waislam bali zilikuwa fikra zilizopandikizwa kutoka nje ya umma. Sheikh Hassan bin Ameir aliwatahadharisha baadhi ya viongozi wa EAMWS kuwa makini na wawe tayari kupambana na kikundi hiki.

Hoja hii ilipoletwa katika ule mkutano ilipingwa na msemaji mkuu alikuwa Bilal Waikela na alieleza chanzo cha fikra ile. Inasemekana serikali haikuwa inaiangalia EAMWS kwa jicho jema na katika kutaka kukata mzizi wa fitna na kuliweka jambo lile wazi iliamuliwa kuwa Rais Julius Nyerere aalikwe kufunga mkutano ule na asomewe risala maalum aelezwe msimamo wa Waislam wa Tanganyika kuhusu EAMWS.

Waikela alimsomea Nyerere risala kali sana kwanza  akieleza mchango wa Waislam katika kupigania uhuru wa Tanganyika, kheri angeishia hapo.

Waikela wakati ule kijana wa miaka kiasi ya 30 akahitimisha risala ile kwa kutoa onyo kuwa Waislam wasichokozwe wakaja kuwasha moto ambao hakuna atakaeweza kuuzima.

Yapata zaidi ya miaka 20 iliyopita Mussa Kwikima alinipigia simu wakati ule niko Tanga akinieleza nia yake ya kuandika historia mgogoro wa EAMWS.

Mimi nilimuhimiza kuandika kwani niliamini Mussa Kwikima atakuwa na mengi ya kueleza kwani yeye ndiye alikuwa katibu wa Tume ya Kuchunguza Mgogoro wa EAMWS. 

Nimeisoma Taarifa ya Mussa Kwikima ambayo aliitoa kwa ‘’Waislam Wote,’’ pamoja na Taarifa ya Fedha. Nilijua lau kama ni miaka mingi imekwishapita lakini yatakuwapo mengi ya Waislam kujifunza katika historia yao.

Ikawa katika kipindi cha takriban miaka 20 iliyopita kila tukikutana au kuzungumza kwenye simu yeye akiwa Tabora mimi niko Tanga lazima tutazungumza kuhusu mswada wa kitabu chake hiki. Mara ya mwisho kuzungumza na Mussa Kwikima ilikuwa majuma mawili yaliyopita alipokuja kunitembelea nyumbani kwangu akiwa kafuatana na mwanae Karama Mussa Kwikima. 


Ilkuwa muda mfupi baada ya Mwalimu Nyerere kuweka jiwe la msingi la Chuo Kikuu Cha Waislam, Chang’ombe huku akiangaliwa na Mufti Sheikh Hassan bin Ameir na Tewa Said Tewa, siku moja RTD ikatangaza kuwa Bukoba inajitoa katika EAMWS.

Hili lilikuwa jambo la kushtusha.
Haikufika hata juma moja, Tanga nayo ikatangaza kujitoa katika EAMWS. 

Rais wa EAMWS Tewa Said Tewa akaitisha mkutano Dar es Salaam wa viongozi wa EAMWS kutoka mikoa yote ya Tanzania kuja kujadili hali ile.

Kilichomtisha Tewa Said Tewa ilikuwa nguvu ya vyombo vya habari RTD chini ya Martin Kiama na The Nationalist chini ya uhariri wa Benjamin Mkapa ulivyokuwa unatangaza mgogoro ule. Habari zilizokuwa zinatolewa zilikuwa ni zile za kundi lililojitenga na zikiandikwa namna ya pekee. RTD na The Nationalist halikutoa nafasi kwa viongozi wa EAMWS kujieleza.

Mkutano wa EAMWS uliuda tume na hapa ndipo alipoingia Mussa Kwikima kijana wakati ule Jaji wa Mahakama Kuu kwa kuombwa atiwe katika Tume ya Uchunguzi wa Mgogoro wa EAMWS iliyokuwa na wajumbe saba.

Mussa Kwikima akawa Katibu wa tume hii.  Wakati huo tayari mikoa 9 ilikuwa tayari imeshajitenga na EAMWS kati ya mikoa 17 iliyokuwapo. RTD na The Nationalist vikawa tayari vimejenga mgogoro ule kufikia hali ya kuonekana kuwa ni mgogoro mkubwa sana Waislam wanawakataa viongozi wabovu na wapinga serikali ndani ya EAMWS.

Hivi ndivyo Mussa Kwikima alivyotumbukia katika kapu ambalo propaganda ilijenga kuwa ni kapu lililokuwa na samaki waliochina.

Ndani ya kapu lile alikuwamo Sheikh Hassan bin Ameir, Tewa Said Tewa na Bi. Titi Mohamed.

Hakuna ambae alikuwa hajui historia za watu hawa katika kupigania uhuru wa Tanganyika. 

Katikati ya mgogoro huu uliokuwa umewatia simanzi watu wa Dar es Salaam mwezi huo wa Oktoba, 1968 Abdulwahid Sykes akafariki dunia.

Msiba wa Abdul Sykes uliwarejeshea watu wa Dar es Salam kumbukumbu nyingi za Nyerere alipoingia mjini na kupokelewa na Abdul Sykes wakikumbuka kumuona akiongozananae wakati mwingine wakitembea kwa miguu pamoja mitaa ya Gerezani, Abdul akimtambulisha Nyerere katika juhudi za kuijenga TANU.

Ule ndiyo ulikuwa wakati TANU inanyanyukia kwa nguvu na watu wa Dar es Salaam walikiunga mkono chama kwa hali na mali.

Lakini miezi ile mitatu ya mwisho ya mwaka wa 1968 mji ulikuwa umegubikwa na hofu. Masheikh wengi kipindi hiki walikuwa wakigongewa milango usiku wa manane na kukamatwa. Hakika huu ulikuwa wakati mgumu.

Kimetokea nini ndani ya EAMWS kiasi cha kukumbwa na haya yote?

Waislam walijiuliza kwa mshangao vipi juzi Nyerere kaweka jiwe la msingi la Chuo Kikuu cha Waislam chini ya usimamizi wa EAMWS leo ghafla viongozi wake kutoka mikoani wanatokea katika magazeti na kusikika  katika radio wakisema hawana haja nayo?

Hili halikuwa jambo rahisi kueleweka.

Waikela alikuwa mmoja wa wajumbe wa Tume ya Kikwima na hakuchelewa alimwonya kijana wake akamwambia, ‘’Mussa hili jambo litakuharibia kazi yako.’’

Nini likukuwa jibu la Mussa Kwikima?

‘’Kazi hii ni ya Allah lazima niifanye kutafuta salama ya dini yangu ikiwa ndiyo itakuwa mwisho wa kazi yangu basi hivi ndivyo Allah alivyoniandikia.’’

Mussa Kwikima alikuwa kijana mdogo wa miaka 29.

Waikela baada ya ule mkutano wa mwaka wa 1963 ambao alimsomea Nyerere ile risala kali, mwaka uliofuatia baada ya maasi ya wanajeshi Januari 1964 alitiwa kizuizini na kufungwa jela ya Uyui huko kwao Tabora.

Waikela alikuwa anajua mengi sana katika mgogoro ule na nini kilikuwa kinatafutwa. Tatizo lilikuwa kwa Waislam kujenga Chuo Kikuu.
Inawezekana Mussa Kwikima hakuwa anayajua mengi katika mgogoro ule hadi hapo baadae kabisa.

Kwikima hakujua kuwa kulikuwa na moto wa makumbi unafukuta chini kwa chini kuanzia mwaka wa 1963 baada ya Muslim Congress mbili ya mwaka wa 1962 na 1963 mikutano ambayo ilikuja na mipango yake ya elimu kwa Waislam mipango iliyopelekea ujenzi wa Chuo Kikuu.

Mwezi Novemba ile Tume ya  Kwikima  ilikwenda kuonana na Waziri wa Habari Hasnu Makame ofisini kwake kumtaka azuie propaganda za RTD na The Nationalist dhidi ya viongozi wa EAMWS.

Hapakutokea mabadiliko yoyote.

Sauti zilizokuwa zikisikika zilikuwa zile zile za wapinzani waliojitenga na EAMWS. Hapo ndipo Tewa Said Tewa na Bi. Titi Mohamed wakaamua kwenda kuonana na Rais Mwalimu Julius Kambarage Nyerere nyumbani kwake Msasani.

Yale waliyoyasikia kutoka kinywani kwa Nyerere hayakuhitaji mkalimani kuyaeleza.

Kama Nyerere alitoka kichwa chini katika mkutano wa EAMWS baada ya kusomewa risala na Bilal Waikela safari hii ilikuwa zamu ya Tewa na Bi. Titi kuondoka nyumbani kwa Nyerere, Msasani vichwa vyao wameinamisha.

Iliwadhihirikia wazi kuwa Nyerere hakuitaka EAMWS katika nchi yake.

Mwezi Desemba kundi lililojitenga likafanya mkutano wao wa kwanza Ukumbi wa Arnautoglo agenda ikiwa kujadili mgogoro wa EAMWS.

Baada ya mkutano huu haukupita muda wakatangaza kuitisha mkutano mwingine Iringa uliopewa jina kuwa ni ‘’Mkutano wa Waislam wa Tanzania.’’

Ilikuwa wazi kuwa mkutano huu wa Iringa ulikuwa na nia ya kuishawishi serikali kuivunja EAMWS na kuunda chama mbadala.

Tume ya Kwikima nayo ikatoa taarifa yake kwa Waislam tarehe 11 Desemba 1968 na ikatangaza kuitisha Mkutano Mkuu wa EAMWS mwezi unaofuatia Januari 1969. Mussa Kwikima alikuwa sasa anakimbilia kutimiza miaka 30 kwani alikuwa amezaliwa tarehe 19 Machi, 1939.

Kwa miezi mitatu mfululizo Mussa Kwikima hakuwa na uwanja ambao angeweza kueleza chochote katika ule mgogoro na sababu ilikuwa vyombo vyote vilikuwa kama vile vimewekwa makhsusi kutumikia wale wapinzani wa EAMWS.

Taarifa ya Mussa Kwikima ilileta matumaini mapya kwa Waislam kuwa labda Tume ya Kwikim sasa itamaliza mgogoro ule na ujenzi wa Chuo Kikuu utaendelea baada ya kutekelezwa kwa mapendekezo ya Tume.

Mategemeo yao makubwa Waislam yalikuwa kwa Sheikh Hassa bin Ameir kwani wapinzani wa EAMWS hawakuwa na kiongozi mwenye hadhi ya Sheikh Hassan bin Ameir.

Aliyoyafanya Sheikh Hassan bin Ameir katika dini na ndani ya TANU yalikuwa hayana mfano wake.

Sheikh Hassan bin Ameir akawa ni kizingiti kikubwa kwa wale waliotaka kufanya mkutano Iringa.

Amri ikatoka kuwa Sheikh Hassan bin Ameir akamatwe.

Kazi ya kukamata   ni kazi ya Jeshi la Polisi. Waziri wa Mambo ya Ndani Said Ali Maswanya alipompa amri IGP Hamza Aziz kumkamata Sheikh Hassan bin Ameir, Hamza Aziz aliuliza kosa alilofanya Sheikh Hassan bin Ameir.

Jibu alilopewa ni kuwa Sheikh Hassan alikuwa anataka kupindua serikali.

Hamza Aziz alijibu kuwa huo ni uongo na akakataa kutii amri ile.
Hili lilikuwa halijapata kutokea.

Usalama wa Taifa wakamkamata Sheikh Hassan bin Ameir usiku nyumbani kwake Magomeni na usiku ule ule akasafirishwa kwao Zanzibar na kuambiwa kuwa asirejee bara maisha yake yote.

Kizingiti kikawa kimeondolewa.

Mkutano uliokusudiwa kufanyika Iringa ukafanywa na ulifunguliwa na Abeid Amani Karume tarehe 13 Desemba 1968.

Mkutano huu ukapitisha katiba ya mpya ya jumuiya ya Kiislam iliyopewa jina la BAKWATA katiba hii ilikuwa sawasawa na katiba ya TANU.

Historia ikawa kama vile imejirudia.

TANU ilinakili katiba yake neno kutoka katiba ya Convetion People’s Party (CPP) ya Kwame Nkrumah.

BAKWATA ikaomba itambuliwe na serikali na ipige marufuku EAMWS.

Bila kuchelewa Mussa Kwikima alitoa taarifa ya EAMWS kuhusu BAKWATA.

Kwikima baada ya siku hii mwaka wa 1968 hakupata tena kuandika maneno ya ukweli kama hayo hao chini hadi anafariki.

Kwikima alisema:

‘’Hakuna anaeweza kutishia kuwepo kwa EAMWS isipokuwa wanachama wake, sheria na serikali, lakini si watu binafsi hata ikiwa mikoa yote 17 ikijitoa haitamaananisha kuwa jumuiya imekufa kwa kuwa kuwepo kwake hakutokani na kuwepo kwa mikoa hiyo kama wanachama isipokuwa kuwepo kwa wanachama wake, Waislam.’’

Mussa Kwikima kabla ya mgogoro wa EAMWS alikuwa ameteuliwa na Rais Nyerere kuwa Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania.

Kwikima ndiye hasa alikuwa nguvu kuu katika Tume ya Waislam ya kunusuru EAMWS.

Baada ya kuundwa kwa BAKWATA Mussa Kwikima alihamishwa kutoka Dar es Salaam na kupelekwa Mwanza kama Hakimu Mkazi na Rais Nyerere akamvua madaraka ya Ujaji.

Laiti angelibakia kama Jaji Mussa Kwikima ndiye angelikuwa Jaji Mkuu wa kwanza mzalendo baada ya kuondoka Philip Telford Georges kutoka Dominica.

Huyu ndiye ndugu yetu Mussa Hussein Hamadi Kwikima.

Tunamuomba Allah amsamehe madhambi yake na alifanye kaburi lake kuwa moja ya mabustani ya peponi.
Amin